kwangila

Just another WordPress.com weblog

SIKUKUU YA KUVUTA MARIJUANA MAREKANI.

Ilikuwa saa kumi na dakika ishirini tarehe ishirini mwezi wa nne. wanafunzi wa chuo kikuu cha Brown walifurika uwanjani kwa madai eti wanasherehekea majilio ya msimu wa joto. Uwanja mzima ulifurika vimwana na maghulamu weupe wengi na weusi wachache. Kama kawaida kwota sketi zilikuwa nyingi huku baadhi ya mibabe wakiwa kifua wazi kuonyesha malaika zao. Busu zilikuwa si haba. za waume kwa waume, wake kwa wake na zingine za waume kwa wake. Kila mtu alionekana mwenye furaha iliyovuka mipaka. Vicheko havikuwa vya kawaida. Ungefika pale ndugu ungedhani wanafunzi jamani wameanza kupagawa. Wachuuzi wa vyakula walikuwa chonjo kuokota dola. Walijua hii ni siku ambayo wanafunzi hula pasipo kuweka breki.

Hali hii isiyo ya kawaida ilinipelekea kuuliza maswali mbona leo wanafunzi wa chuo kikuu wana furaha isokuwa na kifani? Wanafunzi wangu hawakuachwa nyuma pia bali waliniomba rukhsa ya kujumuika na wenzao. Waliita sikukuu ile 4:20 at 4:20 maanake tarehe ishirini Aprili, saa kumi na dakika ishirini. Kwa kawaida niliwajua Wamarekani kama watu wasokuwa na furaha; watu wanaovalia tabasamu kwa muda unapokutana nao; watu waliojawa na upweke kiasi cha kulala vitandani na mbwa wao; watu wasiojumuika na wenzao kwa urahisi labda kuwe ile waiitayo 'appointment'.

Kulikuwepo harufu aina yake katika uwanja mzima. Kila mmoja alionekana kuvuta kitu fulani chenye muundo wa sigara. Moshi wa kile walichovuta ulipeperushwa na upepo mwororo hadi nilipokuwa. Hapo nikajua kuna jambo linaendelea uwanjani. Harufu hii haikuwa ya kawaida. Nilianza basi kuchanganua matukio na kuyaoanisha. Kicheko na vitendo visivyo vya kawaida uwanjani nilivioanishwa na walichokuwa wakivuta wana wa watu. Nilipokuwa mchanga niliambiwa kwamba mtu anapovuta Marijuana huwa na tabia zisizo za kawaida. Mojawepo ya ngano nilizopashwa ni za mvutaji fulani, aliyepika ugali mkubwa kisha akapika 'kijiugali' kingine kidogo eti kiwe kitoweo cha ugali ule mkubwa.

Lakini iwapo hawa wanavuta marijuana mbona basi polisi wamejaa uwanjani? Sikuamini hadi nilpopata habari kutoka kwa Wamarekani zaidi ya watano. Kwamba siku hii inasherekewa takribani katika shule zote nchini Marekani zikiwepo shule za upili pia. Siku hii haiitwi sikukuu hadi wanaoisherehekea wavute Marijuana kupindukia. Eti kusherehekea mwanzo wa joto ni kisingizio tu; swala kuu ni kusokota Marijuana.

Iwapo utajiuliza maswali ndugu basi hivi ndivyo Marekani inawasaidia wafanyibiashara wa Marijuana. Kumekuwepo fununu pia baadhi ya madaktari Marekani wanawashauri wateja wao kutumia Marijuana. Piga hesabu huku ukitilia maanani mamilioni ya wanafunzi wanaovuta marijuana siku hii 'tukufu'. Siku hii pekee imewazalishia walanguzi wa marijuana mabilioni ya dola.  Baada ya kufanya hesabu, jiulize sheria za U.N. zasemaje kuhusu madawa ya kulevya? Juzi Marekani wamevunja sheria ya U.N. na kushambulia Iraq. Hivi jana wamevunja ya madawa za kulevya kwa kuwaruhusu walanguzi kuuza na wanafunzi kununua.

MAREKANI INAOZA KWA KASI NDUGU. 

April 26, 2006 Posted by Daudi Kyeu | Uncategorized | | 4 Comments

UBAKAJI: NJOKI NDUNG’U ANAFICHA HABARI FULANI.

Swala hili lingali halieleweki. Mbunge maalum Njoki Ndung'u amekuwa akijaribu kuwashawishi wabunge wenzake wakubali mswada anaopendekeza; kwamba wabakaji wanastahili kuchukuliwa hatua kali tofauti na jinsi ilivyo sasa. Vikao vingi vimeandaliwa na hivi leo bunge la Kenya ambalo lina wanaume wengi litapitisha au kutopitisha mswada ambao utawafunga wanaume.   

Waitifaki wa mswada huu akiwemo Njoki, wanapokabiliwa na maswali kuhusu mswada wenyewe, habari wanazojitetea nazo ni kama vile ubakaji wa vijisichana vidogo vinapoenda shuleni, ubakaji wa wasichana na wanawake; hivi juzi wamejumulisha habari za kubakwa kwa kinyanya kimoja cha miaka zaidi ya 80. Wanatumia habari hizi kuwafumba wanaume wabunge ili watakapokwenda bunge wapitishe mswada huo mara moja pasi kuupigia maswali.  

Swala fiche ambalo wanawake hawa na baadhi ya wanaume hawataji hata kidogo ni ubakaji wanaosema kwamba umo katika ndoa. Unapochunguza kijelezi cha ubakaji ni kwamba Ubakaji ni kuonyesha dalili au kufanya ngono na mtu pasipo hiari yake au makubaliano; haijalishi mtu yule yumo katika ndoa au la. Ninaposema kuonyesha dalili, ni iwapo utagusa 'vitu' vya mwanamume au mwanamke pasipo hiari yake. Mwanamume akija nyumbani kisha afanye ngono na mkewe pasipo hiari basi huu utaitwa ubakaji. Mwanamume akigusa 'vitu' vya mkewe pasipo hiari yake basi huu utaitwa ubakaji pia.

Hali hii itapelekea wanaume kuwaogopa wanawake maanake ukigusa titi umeingia jela. Aidha wanaume za watu wataishia korokoroni pia kwa sababu waliwakumbatia wake zao au kuwapiga busu pasipo hiari yao. Marekani hivi leo sheria hii inatekelezwa. Madhara yake huku ni kwamba wanaume wamewaogopa wanawake kiasi kwamba mume na mke walioana kwa ndoa takatifu watakuwa na vyumba viwili tofauti vya kulala. Kuna uwezekano kwamba kuzuka kwa ushoga( ndoa za mume-mume au mke-mke) kumesababishwa na wanaume na wanaume kuogopa kuingia jela endapo watagusa 'vitu'.

Ninashuku pia kwamba huyu Njoki Ndung'u anatumiwa kupitisha mawazo ya magharibi barani Afrika. Wametumia nafasi kwamba yeye ni mbunge wa bunge la Afrika na kisha ni mbunge nchini Kenya kupitisha mawazo potovu barani Afrika. Swali ninalojiuliza ni, nani anafadhili vikao vya wabunge kukutania katika hoteli za kifahari ili kupitisha mswada utakaovuruga taasisi ya ndoa.  

Siungi mkono ubakaji wa visichana vidogo au akina nyanya bali ipo haja ya kuongeza katika kijelezi cha ubakaji kwamba ngono katika ndoa halali haitajumulishwa katika kuwatia korokoroni wanaume. Endapo msawada huu utapitishwa pasi kupigiwa maswali kama haya basi wanaume wameangamia. Ni miaka mitano tu na jela nchini Kenya zitajaa wanaume ambao 'wamewabaka' wake zao.

April 26, 2006 Posted by Daudi Kyeu | Uncategorized | | 3 Comments