kwangila

Just another WordPress.com weblog

KITOTO CHA MAREKANI KINASAFIRI ULIMWENGUNI ZAIDI YA MHADHIRI CHUONI AFRIKA.

Kinaya iliyoje? Ukimuuliza mwanafunzi yeyote chuoni Marekani atakwambia ameshazuru Uganda, Uholanzi, Misri, Uswidi na likizo ijayo anaelekea Uhabeshi. Ukimuuliza Mhadhiri wa Sayansi chuoni X katika nchi Y barani Afrika atakwambia kwamba digrii zake zote amezipata nchini Y. Hajawahi hata kusafiri katika mataifa mengine katika bara lake.Ni bayana kwamba nguvu za dola zinawafaidi raia wa mataifa yaliyo na nguvu kiuchumi.

Wahadhiri ni wataalamu ambao wanatakiwa kuwa na uwezo wa kusafiri ulimwengu mzima pasipo kuwekewa vikwazo na ukosefu wa fedha. Hawa ni watu wanaostahili kujua tafiti changa kabisa katika sehemu zingine za ulimwengu.Wakilinganishwa na wahadhiri kutoka Marekani, Wahadhiri wengi barani Afrika ukosefu wa fedha umefungia Wahadhiri katika mazingira ya nchini mwao pekee. Sisemi kwamba hawako radhi kusafiri na kushuhudia tafiti za wengine kote ulimwenguni la hasha, lililopo ni kwamba mishahara wanayopokea haiwaruhusu kushughulikia ya familia kisha waweze kusafiri sehemu mbalimbali ulimwenguni.

Hii ndio sababu vyuoni barani Afrika tunatumia vitabu vilivyotumika karne zilizopita katika kufundisha wanafunzi. Hii ndio sababu Wahadhiri hawa wanatumia mbinu za ufundishaji zilizopitwa na wakati. Wenzao Marekani wakifunza kupitia tekinolojia ya kisasa wahadhiri barani Afrika wangali wanaandaa vikaratasi usiku kabla ya kuhadhiri siku inayofuata.

Aidha mwanafunzi mfanyikazi wa ziada Chuoni Marekani atapata nauli ya ndege kwa mshahara wa mwezi mmoja akilinganishwa na Professa barani Afrika ambaye licha kwamba ana rundo la digrii anasafiri nchi geni mara moja kila baada ya miaka mitano. Hali hii imepelekea Wahadhiri wetu kuwa na mtazamo finyu wa maeneo yao ya Kitaaluma. Kuna hatari hapa maanake elimu isiyokwenda na wakati inawakwamisha raia badala ya kuwasukuma.

Ili kutatua tatizo hili nikidhani wahadhiri wote duniani wanastahili kuwa na kiwango sawa cha mishahara na marupurupu. Ni kwa kupitia njia hii kwamba watakuwa na uwezo wa kusafiri ili kuhudhuria makongamano na kupata habari mpya kutoka kwa wenzao. Nchi nyingi za kiafrika haziwezi kuwalipa vyema wahadhiri wake. Hivyo basi maoni yangu ni kwamba Umoja wa mataifa (U.N.)unastahili kupewa jukumu la kuwalipa wahadhiri.

April 11, 2006 - Posted by Daudi Kyeu | Uncategorized | | 1 Comment

1 Comment »

  1. napenda kujua zaidi lengo la nchi za umoja wa mataifa kusamehe madeni nchi maskini kabisa duniani kama Tanzania ninini?
    Je ninini lengo la bush Rais wa USA kuamua kuingiza watu zaidi ya 50,000 kila mwaka nchini kwake? jambo la green card kwa sasa ni kero kwa wachezaji wengi wa bahati hiyo je hizo sh Ksh 45,000 ambazo wanaitisha watu pale embassy ni za ninini?
    sasa wanasema Visa Processing na Medical kwani basi kwani ikaitwa ni bahati si hata angetoa tiketi bure?
    Willy Msanya
    Arusha

    Comment by William Masai | October 16, 2006


Leave a comment